Hot!

Umuhimu wa rasilimali watu na Huduma kwa wateja



Nilipokuwa safarini rafiki yangu Dotto Bulendu alimuuliza muhudumu kama kuna uwezekano wa kupata kahawa au tangawizi. Huku akiwa amekuja sura (labda kwa kukerwa na swali la bwana bulendu) muhudum alijibu “….kwani wewe unataka nini?..”
Jibu alilopewa bwana doto na mhudumu lilinisikitisha sana. Nilizidi kusononeka sana pale nilipoanza kuitafakari taaluma na ueledi wa usimamizi wa biashara; mathalani nilizidi kutatizwa na na nadharia ya huduma kwa wateja.

Tofauti na wengi tunavodhani, taaluma ya biashara inasisitiza sana kuhusu nadharia za huduma bora kwa wateja hasa pale linapokuja swala la bishara za kuuza huduma kama vile: usafiri, tiba, mawasiliano na kadhalika

Mara nyingi wajasiriamali tumekuwa tukiisahau nguzo hii muhimu ya huduma kwa wateja. Aghalabu utamkuta mtu anakopa hela benki halafu anafanya kila kitu kinachohitajika katika misingi ya biashara isipokuwa tuu rasilimali watu – binadamu anayeajiriwa kwaajili ya kufanya kazi katika biashara ili kutimiza maono ya mwenye biashara.
Katika hali ya kawaida biashara huanza na maono. Ndipo hapo tunaposema malengo na matarajio ya biashara anayajua muanzilishi wa biashara yenyewe. Taaluma ya ujasirimali inashuhudia kwamba bishara mpya itakuwa na uwezekano mkubwa wa kufanikiwa endapo tuu waajiriwa (rasilimali watu) watakuwa wameelewa na kuiamini falsafa ya aliyeanzisha biashara hiyo.

Changamoto kubwa ni kuwa na rasilimali watu ambayo ipo kwa sababu ya uwepo tuu bila kuwa na uelewa wowote kuhusu malengo na umuhimu wa kuifanya biashara husika kuwa endelevu kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Laiti yule muhudumu angejua madhara ambayo yangeweza kutokana majibu aliyomjibu bwana Dotto. Kwa mfano; kwa kupitia tuu marafiki wa Doto, jamii inaweza kuwa na mtazamo hasi kuhusu kampuni husika. Laiti mwenye kampuni hiyo ya usafiri angejua kuwa maono yake ya kutoa huduma bora na kukikisha kuwa wateja wanaridhika na huduma bora inakwamishwa na mhudumu aliyemuajiri.

Ipo haja wajasiriamali kuwa makini na watu tunaowaajiri. Kuna njia nyingi za kuhakikisha kuwa wafanyakazi katika biashara yako wanatembelea falsafa iliyojikita katika maono yako. Semina za mara kwa mara juu ya falsafa ya kampuni ni muhimu. Pia vikao vifupi vya siku kabla na baada ya kazi ni muhimu kwani vinatoa mwanya wa kukosoana na kutambua zaidi uwezo wa watu uliowapa dhamana ya kufanya kazi katika biashara yako.

Mimi na dotto tumemsamehe yule muhudumu lakini tumejiapiza kuwa hatutatumia tena huduma zake. Tumejiapiza kuwa tutajitahidi kusisitiza huduma bora kwa wateja katika maeneo yetu ya kazi. Tumejiandaa kwa changamoto hasa kutoka kwa wafanyakazi wenzetu ambao bado wanaamini kwenye msemo wa chema chajiuza kibaya cha jitemebeza kwa asilimia mia moja.
Sisi tunasema sawa chema chajiuza na kibaya chajiuza ila sio kwa asilimia mia moja. Tunaamini kuwa inawezekana msemo huu ukawa sahihi kwingine. Ila linapokuja swala la huduma kwa wateja ni kwa asilimia kadhaa; cha muhimu ni kutambua kuwa mteja ni mfalme na hakuna biashara/mjasiriamali pasipo mteja.

Amka basi mjasiriamali mwenzangu. Kuwa makini na chaguo katika rasilimali watu katika biashara yako. Usichoke kuwaambia waajiriwa wako kuhusu umuhimu wa kuzingatia falsafa na maono yako. Nakutakia mafanikio katika hilo. Siku nyingine nitakutembelea tujadiliane kuhusu fursa zilizopo na changamoto katika chakula na kilimo. Nitaomba unisaidie kumuuliza rafiki yangu kwa nini ameshindwa kutumia kalamu yake ya uandishi wa habari kuielimisha jamii kuhusu fursa zilizopo katika kilimo.

0 comments:

Post a Comment